"WALIOHUSIKA KUCHOMA MOTO OFISI ZA CHADEMA NI CHADEMA WENYEWE..." TAMKO LA POLISI BAADA YA UCHUNGUZI KUKAMILIKA...

.

Polisi mkoani Arusha imekamilisha uchunguzi wake kuhusiana na kuungua kwa Ofisi za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kusema wanachama wa chama hicho ndio waliohusika. 
 
Hata hivyo, Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema amepinga kauli hiyo na kulipa jeshi hilo siku nne kuwakamata na kuwahoji watuhumiwa watano baada ya kulipatia majina hayo akidai kuwa ndio wanaohusika na uchomaji moto ofisi za chama hicho.
 
“Tumewapatia polisi majina... tunaamini walihusika moja kwa moja la sivyo, chama kitatumia vijana wetu wa Red Brigade kuwakamata na kuwafikisha polisi,” Lema aliwaambia waandishi wa habari jana.
 
Ofisi za Chadema zilizoko katika eneo la Ngarenaro, zilinusurika kuteketea kwa moto juzi baada ya watu wasiojulikana kuwasha moto katika moja ya vyumba vyake.
 
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Japhet Lusinga alisema:
 
“Katika uchunguzi wetu, tumebaini kuwa hakuna mahali palipovunjwa kutoka nje ya uzio na kuruhusu watu kuingia ndani... tumegundua kuna tundu dogo darini eneo la kuelekea bafuni la upana wa futi moja na nusu kiasi haliwezi kuruhusu mtu kupita.
 
“Tumejiridhisha kuwa hakuna mtu anayeweza kupita hapo na ndani tulikuta majivu na baadhi ya vitu vilivyoungua na vifaa vingine.”
 
Lema akiwa na Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Arusha, Ephata Nanyaro alisema: “Tumebaini polisi wanataka kulifanya jambo hili kama la siasa ndiyo sababu juzi badala ya kuanza kuchunguza waliohusika, waliwakamata Mtunza Ofisi na mlinzi wetu na kuwalaza rumande hadi leo (jana) asubuhi kwa madai eti wanawahoji.
 
“Hatukubaliani na taarifa yao, hii ni siasa. Kulitokea mauaji ya bomu, wakasema Chadema wamejilipua, leo ofisi imechomwa wanasema Chadema wenyewe, hili hatukubali, “ alisema.
 
Msajili alaani
Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi amelaani tukio la kuchomwa moto ofisi hizo za Chadema na kusisitiza kuwa wananchi hususan wanasiasa wasiwe wepesi kuingiza hisia kwenye makosa ya kijinai.
 
Alisema kuwa tukio hilo linapaswa kukemewa kwa hali yoyote ile kwa kuwa linavuruga na kuhatarisha amani ya nchi.

ZITTO MATATANI BAADA YA KUSHINDWA KESI YAKE YA KUTOA KASHFA DHIDI YA MFANYABIASHARA RAIA WA AFRIKA KUSINI....


MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema), kwa mara nyingine ameingia matatani baada ya kushindwa kesi iliyofunguliwa na mfanyabiashara raia wa Afrika Kusini.

Katika kesi hiyo, Zitto alituhumiwa kutoa madai kupitia tovuti yake www.zittokabwe.wordpress.com kuwa mlalamikaji, Moto Mabanga alitoa rushwa ya mabilioni ya fedha kwa maofisa wa Serikali ya Tanzania ili kufanikisha kampuni ya Ophir Energy kupata vitalu vitatu vya gesi mkoani Mtwara kati ya mwaka 2004/2005.

Katika kesi hiyo ya madai Namba 153 ya 2013 iliyofunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, mfanyabiashara huyo pamoja na mambo mengine alidai kulipwa fidia ya Dola za Marekani milioni 5 ambazo ni sawa na Sh bilioni 8 za Tanzania.

Katika hukumu iliyotolewa na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Sundi Fimbo, Novemba 21 mwaka huu bila Zitto kuwapo, Mahakama ilijiridhisha kuwa maneno yaliyoandikwa kwenye tovuti binafsi ya Zitto na kwenye mitandao ya jamii yalimkashifu mlalamikaji na mlalamikiwa ameshindwa kuyathibitisha.

Mahakama hiyo imemtaka Zitto kuomba radhi kwenye tovuti yake na mitandao ya jamii ambako aliandika kashfa dhidi ya mfanyabiashara huyo.

Pia imemuamuru mlalamikiwa pamoja na washirika wake kuacha kwa njia yoyote ile kuendelea kuandika na kusambaza habari zenye kumkashifu mlalamikaji.

Mwanasiasa huyo kijana ambaye katika siku za karibu amekumbwa na misukosuko ya kisiasa, pia ameamriwa kumlipa mlalamikaji jumla ya Sh milioni 3 kutokana na madhara yaliyotokana na kashfa husika.

Awali, mlalamikaji alitaka kulipwa Dola za Marekani milioni 5, lakini akashindwa kuithibitishia Mahakama ni jinsi gani alipata hasara ya kiasi hicho cha fedha kutokana na kashfa hiyo. Pia Zitto ametakiwa kulipa gharama zote za kesi hiyo.

Alipoulizwa jana kama anakubaliana na hukumu hiyo au anakusudia kukata rufaa, Zitto alijibu kwa ufupi; “Sijaona hukumu wala sijawahi kufika mahakamani.”

Julai mwaka jana, Mabanga alifikisha malalamiko mahakamani akidai Zitto ameandika taarifa zenye kumkashifu kwa kumhusisha na utoaji mkubwa wa rushwa.

Mbali na kujihusisha na biashara sehemu mbalimbali duniani, Mabanga amekuwa akitumika kama kiunganishi kati ya wawekezaji wakubwa na Serikali mbalimbali ikiwamo Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Katika madai yake, aliitaka Mahakama kumuamuru Zitto kutoka uthibitisho dhidi ya madai ya kuwapa rushwa maofisa wa Serikali katika mchakato wa kupata vitalu vya gesi wa kampuni ya Ophir Energy.

Pia aliiomba Mahakama kutamka kuwa maneno yaliyoandikwa na Zitto ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Fedha kwenye tovuti yake na mitandao ya jamii si ya kweli bali ni kashfa.

Wakati hali ikiwa hivyo, wiki mbili zilizopita Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kilimvua nyadhifa zote Zitto Kabwe ikiwamo ile ya Naibu Katibu Mkuu.
 

Katika mkutano wa Kamati Kuu ya Chadema uliofanyika Dar es Salaam, Mwanasheria Mkuu wa chama hicho Tundu Lissu, alisema Zitto na wenzake wamebainika kukihujumu chama kwa kuanzisha mpango unaoitwa Mkakati 2013 ukilenga kukisambaratisha chama hicho, ili kuwaondoa madarakani Mwenyekiti na Katibu Mkuu wake.

Wengine waliovuliwa nyadhifa zao ni pamoja Dk. Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, ambapo walipewa siku 14 wajieleze kimaandishi kabla ya kuchukuliwa hatua zaidi za kinidhamu ikiwamo kuvuliwa uanachama.

-Mtanzania

DR.KITILA MKUMBO AKANUSHA KUWA MJUMBE WA KAMATI KUU YA CHADEMA,ADAI ALIJIUZULU TANGU MWAKA 2010....

.
 
Katika hali ya kushangaza Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Kitila Mkumbo, amekanusha madai ya kuwa mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA kupitia barua yake aliyouandikia uongozi wa chuo hicho, huku akisisitiza kuwa alijiuzulu nafasi hiyo tangu Januari 2010.

Hiyo imedhibitishwa na taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa Dar es Salaam jana na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo- Utawala na Ofisa Mnadhimu wa Chuo Kikuu, Prof. Yunus Mgaya, iliyoeleza kuwa Dkt. Mkumbo alikanusha kimaandishi tuhuma za kuwa mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA na kwamba tangu alipojiuzulu 2010, hajawahi kurejea wadhifa huo.

Wakati hayo yakiendelea Chuo hicho kimetoa taarifa ya kumsimamisha kwenye nafasi za uongozi ndani ya Chuo hicho, Dkt. Mkumbo na kuanza kuchunguzi dhidi yake, baada ya kuripotiwa kuwa anajihusisha na siasa ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kinyume na waraka wa Utumishi wa Umma wa mwaka 2000.

Taarifa iliyotolewa kwenye vyombo vya habari na kusainiwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo-Utawala na Ofisa Mnadhimu wa Chuo Kikuu, Prof. Yunus Mgaya,ilieleza kuwa kamati ya uchunguzi imepewa jukumu la kuchunguza na kubaini ukweli, kisha kutoa mapendekezo kwa uongozi wa chuo hicho.

“Uongozi wa Chuo utatoa uamuzi kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo,”ilieleza sehemu ya taarifa hiyo ya Desemba 3 mwaka huu. Chuo hicho kimewataka watu watakaohojiwa na kamati ya kumchunguza Dkt. Kitila kutoa ushirikiano wa dhati ili kubaini ukweli na kuharakisha mchakato wa uchunguzi.

Kutokana na hali hiyo, Chuo hicho kimewataka wananchi kuwa na subira kuhusiana na jambo hilo.

Taarifa hiyo, ilieleza kuwa chuo hicho kilipata taarifa kuhusu kuvuliwa uongozi Dkt. Mkumbo ndani ya CHADEMA. “Kwa mujibu wa vyombo vya habari kuwa alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA,taarifa hizo zimeushtua uongozi wa chuo kikuu, kwa sababu zimekuwa tofauti na ilivyokuwa ikieleweka kuhusu uhusiano uliokuwepo baina ya Dkt. Mkumbo na CHEDEMA,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo na kuongeza;

“Uongozi wa chuo unapenda kutoa taarifa kwa umma kuwa kwa mujibu wa Waraka wa Utumishi wa Umma uliotolewa mwaka 2000 ni marufuku kwa mfanyakazi wa umma kuwa kiongozi au kuwa na madaraka yanayofanana na uongozi katika chama chochote cha siasa.”

Taarifa hiyo, ilieleza waraka huo uko wazi na wafanyakazi husika wanaufahamu na wale wanaoonesha dalili za kutetereka, ukumbushwa au kuonywa na wanaokaidi uchukuliwa hatua kwa mujibu wa taratibu zilizopo.

“Kwa msingi huo na kwa kuzingatia kuwa Dkt. Mkumbo hajawahi kujibainisha rasmi kama kiongozi ndani ya CHADEMA, Chuo hakikusita kumpitisha kuwa Mkuu wa Kitivo cha Elimu katika Chuo Kikuu Kishiriki kuanzia mwaka jana,”Ilieleza tarifa hiyo na kuongeza kuwa kabla ya hapo Dkt. Mkumbo alikuwa Mkuu wa Idara ya Saikolojia ya Elimu na Taaluma za Mitaala katika Shule Kuu ya Elimu Kampasi ya Mwalimu Nyerere Mlimani, mwaka 2009 hadi mwaka jana.

Chuo hicho, kimesema pamoja na wingi wa taarifa hizo za vyombo vya habari kuhusu Dkt. Mkumbo, amekanusha kimaandishi tuhuma hizo za kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA na kusisitiza kuwa yeye alijiuzulu nafasi hiyo ya Ujumbe wa Kamati Kuu tangu Januari 2010. Ilielezwa kuwa Dkt. Mkumbo alifanya hivyo baada ya kuelezwa kwa sheria husika na kwamba hajawahi kurejea wadhifa huo.

Dkt. Mkumbo alivuliwa wadhifa wake ndani ya CHADEMA hivi karibuni kutokana na kudaiwa kuandaa waraka wa siri wa kufanya mapinduzi ya uongozi, ambapo tayari amepatiwa mashtaka 11 anayotakiwa kuyajibu ndani ya siku 14 na chama hicho.

Wengine waliovuliwa nyadhifa zao kwa kuhusishwa na waraka huo ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe na aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA mkoani Arusha, Samson Mwigamba

-Majira

PICHA: MKUTANO WA KATIBU MKUU WA CCM AKIHITIMISHA ZIARA YAKE JIJINI MBEYA....

.

Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana akihutubia maelfu ya wakazi wa Mbeya mjini, kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika jana jioni katika Uwanja wa Rwanda Nzovwe, wilaya ya Mbeya mjini, ikiwa ni mkutano wa kuhitimisha ziara yake katika mkoa huo, ya kukagua utekelezaji wa ilani ya CCM, kusikiliza kero za wananchi na kujadiliana nao njia ya kuzitatua.
 Katibu NEC,Itikadi na Uenezi,Nape Nnauye akihutubia maelfu ya wananchi wa Mbeya, katika mkutano wa hadhara uliofanyika jana jioni katika Uwanja wa Rwanda Nzovwe, wilaya ya Mbeya mjini, ikiwa ni mkutano wa kuhitimisha ziara yake katika mkoa huo, ya kukagua utekelezaji wa ilani ya CCM, kusikiliza kero za wananchi na kujadiliana nao njia ya kuzitatua.

 Sehemu ya Wakazi wa jiji la Mbeya Mjini wakishangilia jambo wakati Katibu wa NEC,Itikadi na Uenezi,Nape Nnauye alipokuwa akihutubia katika mkutano wa hadhara uliofanyika jana  jioni katika Uwanja wa Rwanda Nzovwe, wilaya ya Mbeya mjini, ikiwa ni mkutano wa kuhitimisha ziara yao katika mkoa huo.

PICHA:MKUTANO WA DR SLAA KAHAMA MJINI JANA...

.
 
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willbrod Slaa akihutubia wakazi wa Kahama Mjini jana.
Dk. Slaa akiendelea na mkutano uliofanyika kwenye Uwanja wa CDT mjini Kahama  jana.

"MGOGORO ULIOPO NDANI YA CHADEMA NI KAZI YA MAKACHERO..." DR SLAA AFUNGUKA

.

KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa amesema mgogoro uliopo ndani ya chama ni kazi ya makachero. Alitoa kauli hiyo jana jioni alipokuwa akihutubia mamia ya wananchi wa Mji wa Kahama mara baada ya kuwasili akitokea jijini Dar es Salaam akiwa njia kuelekea mkoani Kigoma kwa ziara ya wiki moja.
 

Dk. Slaa ambaye alifika saa 12 jioni alitumia muda dakika zisizozidi 20 kuhutubia ambapo alisema chama hicho kina taarifa za ushiriki wa makachero, lengo likiwa kukidhoofisha na hatimaye kukisambaratisha chama hicho.

“Tunazo tayari taarifa kuwa makachero ndio wapo nyuma ya mgogoro ndani ya chama, wameingia kwa nia ya kutuvuruga, lakini tupo imara.

“Nawasihi Watanzania waache kushabikia vitu visivyo vya msingi, badala watumie muda wao kufikiri na kufanya mambo ya msingi kwa Taifa.

“Yote yanayotokea katika chama chetu kwa sasa yanatuandaa na kutukomaza kwa ajiri ya kuchukua madaraka ya nchi mwaka 2015,” alisema.

Alisema kuwa, wanachama wote wa Chadema wanapaswa kujua hakuna aliye juu ya Katiba ya chama hicho, kwa hiyo Katiba italindwa na kusimamiwa bila woga kwa maslahi mapana ya chama.

Leo anatarajiwa kuondoka na msafara wake kuelekea mkoani Kigoma, ambako kituo chake cha kwanza kitakuwa eneo la Kakonko na baadae ataelekea Muhambwe.

Katika ziara hiyo ya kukagua uhai wa chama atatembelea mikoa ya Shinyanga, Kigoma, Tabora na Singida.

MAHAKAMA YATAKIWA KUMTAMBUA SOKWE KAMA BINADAMU KISHERIA....

.

Kikundi kimoja cha kutetea haki za wanyama nchini Marekani kimeitaka mahakama mojamjini New York kumtambua sokwe kama binadamu kisheria.

Kikundi cha Mradi wa Haki Zisizo za Binadamu (Nonhuman Rights Project) kimetaka sokwe mtu alitwae Tommy kupewa hadhi ya “ubinadamu kisheria” na hivyo anastahili kupata “haki muhimu ya uhuru wa kimwili.”

Kikundi hicho kinapanga kufungua kesi ya aina hiyo wiki hii kwa kiniaba ya sokwe wengine watatu wa mjini New York.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Uingereza, BBC, kikundi hicho kinataka sokwe hao wanne kuachiwa huru kutoka kwenye kizuizi chao.

Kimesema sokwe hao wanapaswa kupelekwa mahali mwanachama na Bustani ya Umoja wa Sokwe Watu wa Amerika ya Kaskazini, kikundi hicho kimesema.

Kikundi hicho kilifungua kesi mahakamani Jumatatu kwa niaba ya sokwe Tommy na ushahidi wa wanasayansi umehusishwa katika kesi hiyo.

“Tunatoa hoja kwamba sokwe ni wanyama wanye utawala wao - yaani, wana uwezo wa kujitegemea kuamua, wenye ufahamu binafsi, na wenye uwezo wa kuchagua jinsi ya kuishi maisha yao,” mwasisi wa kundi hilo, Steven Wise, aliliambia shirika la habari la Marekani, Associated Press.

MAGAZETI YA BONGO LEO 5/12/2013....

MAGAZETI YA LEO
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.

 

Copyright © 2010 GUMZO LA JIJI.

Like Us On Facebook
Follow Us on Twitter